Saturday 28 June 2014

 MAKAMU WA RAISI ALGENTINA ASHITAKIWA


 


Makamu wa raisi nchini Argentina Amado Boudou ameshitakiwa na shitaka la ufisadi.

Bwana Badou anashutumiwa kwa kutumia vibaya mamlaka wakati alipokuwa waziri wa uchumi alipochukua umiliki wa kampuni inayochapisha fedha za Argentina.

Washitakiwa wengine watano pia wameshitakiwa kwa kosa hilo .
Bwana boudou kwa mara kadhaa amepinga mshtaka dhidi yake huku akifutilia mbali wito wa kujiuzulu.Kwa sasa yuko katika ziara ya kibiashara nchini Cuba.

Monday 23 June 2014

WAANDISHI AL JAZEERA WAHUKUMIWA MIAKA 7 JELA



Mahakama nchini Misri imewahukumu jela miaka saba wandishi watatu wa habari wa shirika la habari la Al Jazeera waliokuwa wamezuiliwa kwa miezi sita nchini humo.
Walipatikana na hatia ya kueneza habari za kupotosha na kushirikiana na kundi la wapiganaji wa kiisilamu la Muslim Brotherhood.
Mmoja wa wandishi hao ni Peter Greste, raia wa Australia na ambaye pia alikuwa mwandihi wa habari wa BBC wakati moja.
Hukumu ilipotolewa, Greste kwa hasira aligonga mkono wake katika eneo ambako walikuwa wamezuiliwa huku mwenzake akibururwa kutoka mahakamani na walinzi wa gerezani.

Familia za watuhumiwa nao wakaangua kilio. Kesi hii imelaaniwa sana kote duniani hasa na mashirika ya kutetea haki za binadamu pamoja na mashirika ya habari ya kimataifa.
Lakini nchini Misri, vyombo vya habari vilipeperusha habari hiyo kwa utofauti mkubwa.

Al Jazeera - ni shirika linaloonekana kuunga mkono vuguvugu haramu la Muslim Brotherhood na kwa mtanzamo huo , ni adui wa serikali.
Peter Greste ,ndiye alikuwa anaripoti matukio nchini Misri Disemba mwaka jana wakati wa harakati za mapinduzi.

Kisha yeye na wenzake wawili wakatuhumiwa kwa kusaidia vuguvugu la kigaidi na kutangaza taarifa za kupotosha dhidi ya serikali na maslahi ya taifa hilo.
Madai ambayo serikali ya Australia imekuwa ikikanusha vikali.

Serikali ya Australia ilitoa taarifa yake ikisema kuwa imeshtushwa sana na uamuzi wa mahakama katika kesi ya Peter Greste. Imeelezea kushangazwa sana na hukumu iliyotolewa. Serikali imesema haielewi kabisa matukio haya.

Shirika la Al Jazeera lenyewe limepinga hukumu iliyotolewa dhidi ya wandishi hao, Peter Greste, Mohamed Fahmy na Baher Mohamed likisema kuwa inakiuka sheria.

TAASISI YA AFYA YASHAMBULIWA NIGERIA


Mlipuko umeripotiwa kutokea katika taasisi moja ya umma ya mafunzo ya afya katika mji wa Kano ambao ni wa pili kwa ukubwa nchini Nigeria.

Duru zinasema kuwa idadi ya watu waliojeruhiwa katika shambulizi hilo dhidi ya kituo cha mafunzo ya afya , bado haijulikani.
Mji huo umewahi kulengwa na wapiganaji wa kiisilamu wa Boko Haram, ambao wanataka kubuniwe taifa la kiisilamu Kaskazini mwa Nigeria.

Majimbo matatu Kaskazini mwa Nigeria bado yapo chini ya sheria ya hali ya hatari kufuatia miaka mingi ya harakati za wapiganaji hao wa kiisilamu.


Friday 23 May 2014


 

 WANANCHI WAMLIPUA LISSU KWA KINANA


Wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki, wamemuomba Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, awasaidie kutatua kero zinazowakabili za barabara, elimu na afya.

Wananchi hao wamedai hatua ya kumuomba Kinana awasaidie inatokana na Mbunge wao, Tundu Lissu (Chadema), kuwakataza kuchangia miradi ya maendeleo hali iliyosababisha miradi ya ujenzi wa shule na zahanati kusimama kwa kipindi cha miaka minne.

Wakizungumza jana wilayani Ikungi mkoani Singida, mbele ya Kinana, wananchi hao walisema Mbunge huyo amekuwa akiwakataza kuchanga fedha kwa ajili ya kujenga madarasa na majengo ya zahanati kwa madai kuwa serikali ina fedha za kutosha za kufanya kazi hizo.

“Ndugu Kinana tunaomba utusaidie kwani tangu tulipomchagua Mbunge wetu, Tundu Lissu, hajaendeleza miradi ambayo ilianza kufanywa na Mbunge wa CCM aliyepita, baada ya yeye kutukataza kuchanga aina yeyote ya michango itakayotakiwa na halmashauri kwa ajili ya maendeleo, tumeendelea kuwa katika hali ya ufukara” alisema Omary Lissu mkazi wa kijiji cha Unyanghumpi.

Alisema tangu wamekatazwa kutoa fedha za miradi hakuna kazi ambayo imeendelea hasa katika zahanati Kimbwi ambayo walitarajia iwe imeanza kutumika tangu mwaka 2011 lakini hadi sasa bado haijakamilika na kwamba diwani wao amekuwa akiwashinikiza kutoshiriki shughuli hizo.

Naye Mwalimu wa Shule ya Msingi Unyanghumpi, Juliana Joseph, ambaye anafundisha darasa la awali, alisema tangu madarasa hayo yajengwe kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, mpaka sasa hakuna majengo mengine mapya wala ya zamani kumaliziwa hali inayowafanya baadhi ya wanafunzi kusoma katika darasa ambalo halijaezekwa.

“Ni mwaka wa nne nafundisha katika darasa hili ambalo halina paa,  na mvua inaponyesha inatubidi tusiudhurie vipindi. Mbunge wetu na diwani walitoa tamko la kuwataka wananchi wasichangie umaliziaji wa jengo ndiyo maana hadi sasa tuko hapa, wala hajawahi kufika kutoa msaada wowote,” alisema Joseph.

Alisema darasa la awali lina jumla ya wanafunzi 135 ambao wote wanakaa kwenye vumbi kwani hakuna madawati na vifaa vingine kama dhana za kufundishia. Mkazi mwingine alisema wamekuwa wakipata tabu ya kufuata huduma ya afya katika kijiji kingine wakati kijijini hapo kuna zahanati ambayo imejengwa inasubiri kukamilika.

Akizungumza na wananchi hao katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Makyungi, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema kiongozi bora ni yule anayechangia maendeleo ya wananchi na siyo kuwakataza wananchi kufanya maendeleo.

Alisema Tundu lissu anafanya mambo ambayo hayaendani na matarajio ya wananchi kwani walimchagua wakiamini ataleta maendeleo badala yake anazuia maendeleo. Kwa upande wake, Kinana, alimtaka Lissu kuacha porojo za majukwaani na arudi kwa wananchi kuwatimizia ahadi alizotoa kwani anafedha nyingi anazopatiwa bungeni.

Alisema wilaya ya Ikungi iko nyuma kimaendeleo ikilinganishwa na wilaya nyingine nchini sababu kubwa ikiwa ni mbunge mwenyewe ambaye ameshindwa kupigania maendeleo ya jimbo lake na badala yake amekuwa akigombana na kila mtu serika
lini.

  UN YASEMA VATCAN INAPUUZA HAKI ZA WATOTO


 PAPA FRANCIS

Kamati ya Umoja wa Mataifa dhidi mateso imelaumu vikali kanisa Catholiki kwa kutoshughulikia ipasavyo suala la unyanyasaji wa watoto ndani ya kanisa hilo.
Katika ripoti iliyochapishwa hivi karibuni na Umoja huo mjini Geneva , Kamati hiyo imeushutumu utawala wa Vatcan kwa kuwahamisha watawa kutoka parokia moja hadi nyingine kuwaepusha kushtakiwa, na kupuuza haki za waathiriwa za kupokea fidia .
Utawala wa Vatican uliithinisha mkataba dhidi ya unyanyasaji , ukatili na matendo yaliyo kinyume na utu.Uchunguzi uliofanywa na kamati ya Umoja wa Mataifa dhidi ya Vatcan ni sehemu ya uchunguzi wa mara kwa mara wa kamati hiyo dhidi ya nchi wanachama ili kuhakikisha mikataba inatekelezwa.

Kamati hiyo ya Umoja wa Mataifa ina hofu kuwa wakati utawala wa Vatcan umeelezea kutokubali kamwe kuwepo kwa unyanyasaji ndani ya kanisa, maneno hayaendani na vitendo .

Kamati hiyo imekasirishwa zaidi na kwamba Utawala wa Vatcan unasisitiza kuwa unahusika zaidi na wahudumu wanaofanyika kazi ndani ya Vatcan kwenyewe , kuliko makasisi wake wanaofanyika kazi kwingineko duniani.

Mwezi Januari mwaka huu utawala wa Vatcan ulichunguzwa upya na kamati ya Umoja wa Mataifa kuhusu haki za watoto, baada ya kupokea ukosoaji kama huo kwamba ulishindwa kuwalinda watoto waliokuwa chini ya uangalizi wake.

 GERMAIN KATANGA JELA MIAKA 12

Germain Katanga

Mahakama ya kimataifa ya jinai ICC imemhukumu kiongozi wa zamani wa wanamgambo waasi katika Jamuhuri ya kidemokrasi ya Kongo, Germain Katanga, kifungo cha miaka kumi na miwili jela baada ya kumpata na hatia ya uhalifu wa kivita. 
 
Bwana Katanga alipatikana na hatia ya kuhusika katika mauaji ya mamia ya wanavijiji katikaeneo la Ituri Katanga mwezi Machi mwaka 2003.

Jimbo la Katanga ni jimbo lenye utajiri wa madini ya dhahabu kaskazini mashariki mwa nchi hiyo . Lakini kiongozi huyo wa waasi mwenye umri wa miaka thelathini na sita hakupatikana na hatia ya kuwatumikisha watoto vitani na makosa mengine ya ubakaji.

Monday 28 April 2014

 MZOZO WA KIDIPLOMASIA
 KATI YA KENYA NA SOMALIA


Mzozo wa kidiplomasia unanukia kati ya Kenya na Somalia baada ya polisi kumkamata kimakosa mmoja wa maafisa wakuu wa ubalozi wa Somalia nchini Kenya Siyad Mohamud Shire .

Tayari balozi wa Somalia nchini Kenya Mohamed Ali Nur ameitwa na serikali yake kueleza matukio yanayoambatana na kukamatwa kwa raiya wa asili ya kisomali ambao serikali inasema baadhi yao hawana vibali vya kuishi nchini.

Maafisa wa polisi nchini Kenya wamekuwa wakiendelea na msako wao dhidi ya wahamiaji haramu na wale wanaoshukiwa kushiriki matendo ya kigaidi na uhalifu.
Hata hivyo serikali ya Somalia imesikitishwa nao kwa kumkamata afisa wa ubalozi wa Somalia anayeshughulikia masuala ya kisiasa Siyad Mohamud Shire.

Kwa sababu hiyo Somalia imetuma taarifa katika vyombo vya habari ikisema kuwa waziri mkuu Abdiweli Sheikh Ahmed amefanya mazungumzo na balozi wa Somalia nchini Kenya aliyefika Mogadishu hapo Jumapili kumweleza hatma ya raiya wa Somalia wanaoishi Kenya katika msako unaoendelea.

Japokuwa serikali ya Kenya kupitia kwa wizara ya usalama wa kitaifa imekuwa ikishikilia kuwa hailengi jamii yoyote katika kuwakamata raiya wa kigeni na kuwarejesha katika nchi zao ama kambi za wakimbizi.Taarifa hiyo imeanusha hilo na kusema maafisa wa polisi wamekuwa wakiwazuilia wasomali wengi na kuwatesa.

Tukio la kumnasa, Bwana Siyad Mohamud Shire limechukuliwa na serikali ya Somali kuwa ukiukaji mkubwa wa mkataba wa kidiplomasia.Inasemekana kuwa bwana Shire alikamatwa na kuzuiliwa na polisi kwa muda licha ya kuwa na kitambulisho cha kazi.

Mkutano kati ya waziri mkuu wa wa Somali na balozi wa Kenya ulifanyika baada ya baraza la mawaziri kuandaa kikao kisichokuwa cha kawaida kujadili hali ilivyo Kenya.

Juhudi za kumpata waziri wa mambo ya nje wa Kenya balozi Amina Mohamed kueleza msimamo wa serikali hazikufaulu ila maafisa wa polisi walikataa kuzungumzia suala hilo wakisema kuwa litashughulikiwa na ngazi ya juu.

Polisi nchini Kenya walianza msako kote nchini wiki tatu zilizopita baada ya matukio mengi yanayoambatanishwa na ugaidi ama uhalifu kutokea huku zaidi ya watu kumi wakifariki baada ya milipuko kadhaa kutokea katika mtaa wa Eastleigh na maeneo jirani jijini Nairobi.

Kisichojulikana kwa sasa ni namna nchi zote mbili zitakavyoendelea kushirikiana kidiplomasia katika mazingira yaliyopo.